Alhamisi, 9 Julai 2015

MKUU WA WILAYA SONGEA, AMALIZA MGOGORO WA MUDA MREFU WA ARDHI HUKO MSHANGANO-SONGEA
Mkuu wa Wilaya ya Songea Profesa Norman Sigalla 'King'

Na   Andrew  Mhaiki, Mwanaperamiho blog

MKUU  wa wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma, Profesa  Norman  Sigalla” King’  amemaliza  mgogoro  wa muda  mrefu  wa kugombea  ardhi  eneo  ambalo  lilitengwa  kwa ajili  ya ujenzi  wa shule ya msingi na  kulirejesha  mikononi mwa wananchi  wa kata  ya Mshangano   katika  Manispaa ya  Songea mkoani hapa.

Wananchi  hao  waliingia  kwenye  mgogoro  wa kugombea ardhi   hiyo  na mmiliki  wa hoteli  ya Top One  Inn, Pascal  Msigwa  ambaye  inadaiwa walibadilisha  matumizi  na  kumpimia eneo hilo  na kumilikishwa  na  Manispaa  ya Songea 

Wakizungumza  na  Mwanaperamiho juzi  Mwenyekiti  wa Serikali  ya  mtaa huo, Samweli  Mbano  alisema  kuwa  Serikali  kupitia  Kamishna  wa ardhi  nchini  waliingia  mkataba  na kampuni  ya ardhi  Plan  kuja   kupima  maeneo  ya kata  hiyo  ya Mshangano  kwa kutenga  maeneo  ya makazi  na huduma  za kijamii.

Alisema  kampuni  hiyo ya  ardhi  Plan  ilipima eneo  hilo  lenye  ukubwa wa  hekta  2.591,  ploti  namba  911  mwaka  2010 ambalo  lilitengwa  kwa ajili ya ujenzi  wa shule ya msingi katika mtaa huo  wa  Mshangano ambapo  wamekaa kusubiri  ofa  yao  kutoka  Manispaa  hiyo  ili waanze  kazi  ya  ujenzi  wa shule  yao, alidai  cha  ajabu  eneo hilo  wananchi  wamepokonywa   na kumilikishwa  mfanyabiashara   ambaye  amekuwa akiwaonyesha  kiburi  cha fedha.

Alisema  wananchi  wa kata  hiyo  walichukua  uamuzi  wa kulitenga  eneo  hilo  kutoka shule  ya msingi, Luhira  iliyopo  katika kata hiyo  kukabiliwa  na msongamano  wa wanafunzi  ambapo katika chumba  kimoja cha  darasa  wanasoma  zaidi  ya  wanafunzi   100 walidai  kitu  ambacho  kimekuwa  kikishusha  maendeleo 
 yao ya   masomo  ya  darasani.

Alisema  wakati  wakiendelea  kufuatilia  ofa yao ili waanze  ujenzi  wa shule yao  ya msingi, walishangaa  kuona   kiwanja  hicho  uongozi  wa ardhi  wa  Manispaa  hiyo   umemmilikisha   mfanyabiashara   huyo anayemiliki hoteli  ya Top  One  Inn  ya mjini hapa, Pascal  Msigwa  ambaye  tayari  alianza  ujenzi  katika kiwanja  hicho  kwa  kujenga  nyumba  na  wananchi  wa  mtaa huo   kwa  pamoja  waliandamana  kwa  hasira  na kwenda  kubomoa  kwa  lengo  la kuusubiri  uongozi  wa idara  ya ardhi  ikiwemo  Mkurugenzi,  Zacharia Nachoa  ili waweze  kuwacharaza  viboko kama  watakwenda  katika eneo  hilo.

Alisema  wananchi  wa mtaa huo  walikuja kupandwa  na hasira  kutokana  na usumbufu   waliokuwa  wakiupata  wa kufuatilia  suala  hilo  kwa uongozi  wa Manispaa  hiyo  bila ya mafanikio  wakati  mfanyabiashara huyo  akiendelea  na ujenzi , huku  watoto  wao  wakiwa wanateseka  kwa  kusoma   kwa kurundikana  katika chumba  kimoja cha darasa  wakati  eneo lao limeporwa  na mfanyabiashara huyo.

Mwenyekiti, Mbano  alisema  kabla ya  wananchi  hawajuchukua  sheria  mkononi  ya kuandamana  na kwenda  kuvunja  kwa kubomoa  ujenzi  wa  nyumba ya  mfanyabiashara huyo ambayo ilikuwa  ikijengwa  katika  kiwanja  hicho  ambacho  kilitengwa kwa ajili ya ujenzi  wa shule ya  msingi katika  mtaa  huo wa Mshangano,  uongozi  wa Serikali  ya mtaa huo  ulimwita mfanyabiashara  huyo, ambaapo  alikaidi kwa  madai  kiwanja  hicho  ni mali  yake  na amekipata  kihalali.

Alisema  walipofuatilia  zaidi  waliweza  kubaini  kiwanja  hicho  kimepimwa  zaidi ya mara moja  akiwemo   mmiliki  wa Top  One Inn  VTC, Msigwa  ambaye  amekabidhiwa  Ofa  na kumilikishwa  kinyume  cha sheria  na  Manispaa hiyo  kupitia  faili  lenye  namba  STC  27243/ MKN  kiwanja  namba 48 ambacho  kimetolewa  Januari, 18, 2013  chenye  ukubwa wa  m2 24,000 ambacho  leseni  yake  inaonyesha  kwa  ajili ya  makazi  ambacho  amelipia  gharama  fedha  taaslim  Sh. 650,000  hadi  kuja  kukipata  na  kuweza  kukimiliki .

Mmoja  wa wananchi  wa  mtaa  huo wa Mshangano,  Emilian  Haule  alipohojiwa  na Mwanaperamihoblog alisema  maamuzi   yaliyotolewa  na   Mkuu wa wilaya  hiyo ya Songea, Profesa  Sigalla” King” yamekuwa  sahihi  na wanampongeza  ya kuwarejeshea  kiwanja hicho  mikononi   mwa wananchi  wa  Mshangano   na  imekuwa  mfano kwa viongozi  wengine  hasa  viongozi  wa Manispaa hiyo ambao  wamekuwa wakifanya kazi  kwa mazoea  badala  ya kufuata  misingi ya kisheria  wanapotoa maamuzi.

Naye   Meneja  wa  Ardhi  Plan  mkoani  Ruvuma, Francis  Mwafyoma   alipohojiwa  na alisema  kufuatia  sheria  ya  ardhi   4/1999 ambayo  inasimamiwa na Kamishina  wa ardhi nchini  alidai  eneo  hilo  linalogombewa   kati ya  Top One Inn  VTC na  wananchi  wa Serikali  ya mtaa wa Mshangano  alidai  uamuzi  uliotolewa na  Mkuu wa wilaya, Profesa  Sigalla  “King” umekuwa  sahihi  utasaidia  kuondoa urasimu  na ubabaishaji  kwa viongozi  wa Manispaa ya Songea

Hata  hivyo  Mmiliki  wa Top One Inn  VTC, Bw. Pascal  Msigwa alipohojiwa  kwa njia  ya simu yake  ya kiganjani   yenye  namba  0754353672  alikiri  kuwepo kwa mgogoro kati yake  na wananchi  wa mtaa wa  Mshangano  wa kugombea  kiwanja  ambacho  ni mali yake  na anakimiliki  kisheria kutoka mwaka  2013.

Kwa upande  wake Mkurugenzi  wa Manispaa hiyo ya Songea, Bw. Zacharia Nachoa  alipotafutwa  ofisini  kwake  ili aweze  kuelezea  sakata  hilo hakuweza kupatikana  baada  ya kuambiwa na mmoja  wa watumishi  katika  ofisi  hiyo  yupo nje  ya  ofisi  kwa kazi ya  ukaguzi  wa ujenzi  wa  vyumba  vya  maabara kwenye  shule  za Sekondari, huku  Ofisa ardhi  Mteule wa Manispaa hiyo, Andason  Mwamengo  ameahidi  kupambana  na wananchi   hao   wa Mshangano, licha  ya Mkuu wa wilaya  hiyo  kumaliza tatizo  hilo  kwa kurejesha  ardhi  hiyo  mikononi  mwa wananchi.

Mkuu wa wilaya hiyo ya Songea, Profesa  Norman  Sigalla” King”  alipohojiwa   ofisini  kwake  jana  juu ya sakata  hilo la kugombea  kiwanja  kati  ya wananchi  wa Mshangano na mfanyabiashara huyo alisema  baada ya  kukaa  na viongozi  wa Manispaa  na wananchi  wa  Mshangano  meza  moja  na kufuatilia  nyaraka za pande zote  alidai  Msigwa hakufuata  taratibu  za kisheria  katika  kukipata  kiwanja hicho.
MWISHO



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni