Jumapili, 21 Juni 2015

PAULO MALDINI: BEKI MSTAARABU ZAIDI AMBAYE HAKUWAHI KUPATA KADI NYEKUNDU UWANJANI
Image result for PAOLO MALDINI

Na Oswald Ngonyani

Mchezo wa mpira wa miguu maarufu kama soka bado umeendelea kuwa mchezo pendwa kwa watu wengi zaidi kote duniani na hata kuizidi michezo mingineyo kinaganaga. Ni mchezo unaopendwa na watu wa kariba zote.

Kutokana na mchezo huo kuhusudiwa na watu wengi zaidi tayari kumekuwepo na wachezaji fulani fulani ambao kwayo wamejipatia umaarufu mkubwa kutokana na uwezo wao ndani ya dimba. Wachezaji hhawa wapo wengi sana lakini kwa leo nitamzungumzia mchezaji wa nafasi ya ulinzi ambaye enzi zake aliwahi kuwakonga mashabiki wengi wa wa mchezo wa soka.

Namzungumzia muitaliano Paulo Maldini ambaye majina yake kamili ni Paolo Cesare Maldin aliyewahi kuwa mchezaji wa kariba ya juu zaidi katika mawanda ya soka la kimataifa akicheza katika nafasi ya ulinzi wa pembeni (left back) au nafasi ya ulinzi wa kati (central defender). Alizaliwa tarehe 26 Juni mwaka 1968 huko Milan nchini Italia. Katika enzi zake alihudumu katika misimu 25 akisakata kabumbu katika Ligi Kuu ya nchini Italia maarufu kama Serie A.

Ana kimo cha mita 1.86 akiwa ni Baba wa watoto wawili Christian Maldini na Daniel Maldini. Alistaafu kuichezea timu yake ya Taifa mwaka 2002 ambapo katika nyakati zake za kuuchezea mpira aliweza kukiongoza kikosi cha Italia kwa miaka 8 akiwa kama nahodha wa timu hiyo iliyowahi kutwaa ubingwa wa kombe la dunia mara nne. Anaaminika kuwa mlinzi bora zaidi wa miaka yote katika soka la dunia.

Aliwahi kupata tuzo ya UEFA ya mlinzi bora wakati akiwa na miaka 39 lakini pia tuzo ya mlinzi bora wa Ligi ya Serie A mwaka 2004. Mara kadhaa jina lake liliwahi kujumuishwa katika kikosi cha wachezaji bora wa dunia na hata kuzidi kuchagiza ukulu wake katika mawanda ya usakataji wa kabumbu.
Image result for PAOLO MALDINI


Akiwa ndiye beki bora zaidi katika enzi zake, ni vigumu kuamini kuwa mlinzi huyu kisiki hakuwahi kutwaa tuzo ya Ballon d’Or hasa mwaka 1994 ambapo akiwa na AC Milan aliiwezesha klabu hiyo kutwaa Serie A, Supercoppa Italiana, Ligi ya Mabingwa Ulaya na UEFA Super Cup, lakini hakupewa tuzo ya Ballon d’Or. Mwaka huo huo aliiongoza Italia kushika nafasi ya pili katika Fainali za Kombe la Dunia na kutangazwa kuwa mchezaji bora wa dunia na gazeti la World Soccer, lakini tuzo ya Ballon d’Or ilichukuliwa na raia wa Bulgaria, Hristo Stoichkov aliyekuwa akiichezea klabu ya Barcelona.

Mwaka 2002 alishiriki kwa mara ya nne fainali za kombe la dunia na fainali za pili akiwa kama kapteni wa timu yake ya Taifa ni katika mwaka huo Maldini alikuwemo katika kikosi cha wachezaji 11 waliochaguliwa kuunda kikosi cha dunia kilichojulikana kwa jina la ‘FIFA World Cup dream team”

Ndani na nje ya uwanja wachezaji wenzake walimchukulia Maldini kama kiongozi wao. Si katika timu yake ya Taifa pekee lakini pia katika klabu yake aliyowahi kuichezea kwa mahaba makubwa AC Milan ambapo mpaka sasa mashabiki wa klabu hiyo wangali wakimkumbuka.

Ni mchezaji wa kiwango cha kimataifa aliyecheza soka lake katika klabu moja pekee. Alishinda mataji 26 wakati wa uchezaji wake wa muda wa misimu 25. Mlinzi mwepesi, mgumu kupitika aliyekuwa na uwezo wa hali ya juu wa kufanya maamuzi sahihi awapo uwanjani.

Anashikilia rekodi ya kucheza michezo mingi ya michuano ya  Vilabu Ulaya akiwa amecheza michezo 174, ikiwa ni pamoja na kufunga goli la mapema zaidi katika fainali ya Ligi ya mabingwa Ulaya mwaka 2005 goli la sekunde ya 50 katika mchezo dhidi ya Liverpool, mchezo ambao pamoja na timu yake ya AC Milan kutangulia kwa goli 3-0 mwisho wa siku uliamuliwa kwa mikwaju ya penalti baada ya akina Steven Gerald kusawazisha magoli hayo na baadaye kuutwaa ubingwa huo.
Image result for PAOLO MALDINI

Maldini amewahi kuvaa medali tano za European Cup katika miaka ya 1989, 1990, 1994, 2003 na 2007 kitu ambacho si kidogo katika mawanda ya usakataji wa kabumbu kwa mchezaji yeyote yule. Alikuwa ni mmoja kati ya walinzi bora zaidi katika historia ya Ligi ya mabingwa Ulaya  lakini pia alikuwa akivutia sana kutokana na ukweli kwamba alipokuwa na mpira ilikuwa ni vigumu kumdhania kuwa ni yeye  kutokana na ukweli kwamba staili yake ya kiuchezaji haikutofautiana na mchezaji wa sehemu ya kiungo.

Ikumbukwe kuwa kama si George Weah wa Liberia kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa dunia mwaka 1995 basi huenda tuzo hiyo ingekwenda kwa Paulo Maldini ambaye alishika nafasi ya pili huku Jurge Klinsmann wa Ujerumani akishika nafasi ya tatu.

Ni miongoni mwa wachezaji waliowahi kuifanyia makubwa timu ya Taifa ya Italia kama ilivyo kwa akina Dino Zoff, Paolo Maldini na Silvio Piola. Ukulu wake katika usakataji wa ‘Gozi la Ng’ombe’ ungali ukikumbukwa tena na tena na wanafamilia wa mchezo wa soka ulimwenguni kote.

Alikuwa na kipaji cha pekee ndani ya dimba ambapo mbali na sifa zote nilizozielezea hapo juu, Maldini alikuwa na uwezo wa kutumia miguu yote miwili (wa kulia na kushoto) kama ilivyo kwa akina Andreas Brehme, Pavel Nedvěd, Toni Kroos, Adriano Correia na Julian Draxler ambao Mwenyezi Mungu aliwapa uwezo wa kutumia miguu yote katika kuuchezea mpira.

Kuna mengi sana ya kuandika kuhusu mlinzi huyu maarufu ambaye kwa bahati mbaya hakuwahi kushinda tuzo ya mchezaji bora wa dunia. Lakini kikubwa zaidi ambacho kinapaswa kukumbukwa ni historia yake nzuri kuhusu mchezo wa soka, historia iliyotukuka, historia ambayo inazidi kuchagiza ukulu wake tena na tena, historia ya kucheza kandanda pasipo kupata kadi nyekundu mpaka anastaafu.
Naomba kuwasilisha…..



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni