Jumanne, 14 Julai 2015

UMEFANYA MENGI  IKER CASSILAS, DUNIA ITAKUKUMBUKA DAIMA DUMU

Na Oswald Ngonyani

Image result for iker casillas

Kinaweza kikawa kipindi kigumu zaidi kwa mashabiki wengi wa klabu kongwe na tajiri ya nchini Hispania, Real Madrid, klabu ambayo ilianzishwa mwaka 1902 na kujikusanyia idadi kubwa ya mashabiki pande zote za dunia.

Pengine ukongwe na umaridadi wa klabu hiyo ni miongoni mwa vitu vingi vilivyo nyuma ya siri ya kuwa na upana wa mashabiki lakini umaarufu na uwezo wa wachezaji wake ndani ya dimba ni sababu nyingine yenye mashiko zaidi.

Binafsi ninaweza kuandika mambo kadha wa kadha kuhusu ukulu wa klabu ya  Real Madrid, lakini sitakuwa muungwana iwapo sitamtaja mlinda mlango mahiri wa muda mrefu wa klabu hiyo na timu ya Taifa ya Hispania, Comrade Iker Cassilas.

Shujaa huyu wa muda mrefu pale jijini Madrid hayupo katika wakati mzuri kwa sasa. Ni wazi kuwa shaka yake juu ya kinachoendelea klabuni hapo kwa sasa hivi inachagizwa na uwepo wa Mwalimu mpya klabuni hapo, Rafael Benitez.
Image result for iker casillas

Mwalimu huyu aliyekabidhiwa mikoba yote ya Carlo Ancelotti ameonekana kuwa sababu ya hiki kinachuzungumzwa sasa kuwa nyanda huyu ni lazima aondoke klabuni hapo ili magolikipa wengine chipukizi waweze kutua klabuni hapo na hata kuenenda na mifumo inayotakiwa chini yake.

Ni ukweli ulio wazi kuwa huwezi kuyazungumzia mafanikio ya sasa ya klabu ya Real Madrid pasipo kumzungumzia mlinda mlango huyu ambaye kwa muda mrefu sasa ameitumia vema kandarasi yake ya mchezo wa soka akiwa na klabu hiyo.

Ni ngumu sana kwa mchezaji yoyote duniani kufikia ndoto nyingi na kubwa kama ilivyo kwa Casillas. Lakini kwa bahati mbaya sana nyanda huyu anakwenda kuihama klabu hiyo aliyoitumikia kwa mahaba makubwa huku akiwa hajatimiza ndoto moja ambayo alikuwa amejiwekea ndani ya moyo wake.

Nakumbuka wakati fulani kwenye mahojiano fulani ambayo yalifanyika mwaka uliopita (Oktoba 2014) ilithibitika kwamba Cassilas alikuwa na ndoto kubwa katika maisha yake, ndoto ya kucheza soka ndani ya Madrid na kumaliza hapo hapo.

Alizungumza maneno haya “Real Madrid ni nyumbani kwetu, Sikuwahi kuwa na majirani sana au hata vikundi vya shuleni. Nilikuwa na miaka 8 nilivyoanza kucheza mashindano na wakati nina miaka 9 walinisaini. 

Nilikuja hapa kwa hatua na napaona hapa ni nyumbani kwetu. Siku zote nimekuwa sehemu ya Madrid na nimekuwa kama mchezaji na binadamu wa kawaida kwa malezi ya hapa hapa. Mimi nimekuwa hapa na kuwa na kumbukumbu zote hapa hapa”

Iker alisema kwamba sio rahisi na vigumu kumuona yeye akiwa ndani ya jezi ya timu nyingine, “Ni vigumu kufikiria mimi katika timu nyingine. Nitastaafu mpira nikiwa hapahapa. Japokuwa ningependa kujaribu ligi nyingine ili niweze kujua changamoto za kwingineko lakini kwangu mimi Madrid ni chaguo la kwanza zaidi kwani huko hakutakuwa kama hapa.”
Maneno tajwa ya hapo kati yanaonyesha namna ambavyo mwanandinga huyu mwenye miaka 34 alivyo katika ‘dilemma’ hivi sasa kwani mabadiliko ya Kocha yanaonekana kuikatiza ndoto yake ya siku nyingi tangu anajiunga na klabu hiyo miaka 25 iliyopita.

Ni wazi kuwa nyuma ya kila kinachoendelea hivi sasa kuhusu golikipa huyu yupo mtu mmoja ambaye Uongozi mzima wa Klabu ya Real Madrid umemuamini, mtu huyu si mwingine bali ni Kocha mzawa aliyekulia klabuni hapo Rafael Benitez Maudes maarufu kwa jina la Rafa Benitez.

Hapana shaka kuna kitu kimoja kipo ndani ya ubongo wa Mwalimu huyu, kitu ambacho ni vema mashabiki wengi wakakijua ili kutokosa majibu pale watakapoona mchezaji wao kipenzi Iker Cassilas anaenenda zake.

Kwa miaka nenda rudi kumekuwepo na dhana ya wachezaji fulani kuwa ndio mhimili wa klabu hiyo, mhimili ambao kwayo umekuwa ukipewa sana nafasi katika vichwa vya bodi nzima ya Ukurugenzi wa klabu hiyo lakini pia mashabiki husika.
Image result for iker casillas

Wapo wachezaji wengi ambao wamewahi kupitia katika ukulu huu pale Madrid. Miongoni mwa wote waliwahi kupikwa katika chungu hiki cha kutukuzwa yupo pia Iker Cassilas ambaye sasa hivi ustahimilivu wake pale Madrid upo shakani.

Ni ukweli uli wazi kuwa Cassilas ambaye alikabidhishwa kofia hiyo ya ukulu kutoka kwa mkongwe wa siku nyingi wa klabu hiyo Raul Gonzalez, yu mbioni kuondoka zake, sababu ni moja tu, hajawa chaguo sahihi la Benitez.

Ndoto yake haitaweza kutimia tena. Ilianza kuyumbishwa tangu enzi za Jose Mourinho, kwa bahati nzuri akaja Carlo Ancelotti ambaye alimfanya kuwa golikipa wa chaguo la kwanza katika mechi za mashindano makubwa kama UEFA na Copa De Ley nafasi ambayo aliifanyia mambo makubwa na hata kuzidi kujiongezea sifa ya kuaminika klabuni hapo.

Baada ya miaka 25 ya kukaa kwenye klabu yake hiyo hatimaye siku zake kwenye timu hiyo zimetimilika. Kipa huyu ambaye alikuwa kwenye tetesi nyingi za kuhama klabuni hapo nafasi yake kwa sasa ni ndogo sana klabuni hapo.
Image result for iker casillas

Ripoti za uhakika ni kwamba Real Madrid na F.C Porto wamefikia makubaliano ya msingi na na ni wazi kuwa msimu ujao wa Ligi atacheza soka yake nchini Ureno.

Kwa vyovyote vile ni wazi kuwa mpambanaji huyu wa miaka mingi pale Madrid itampasa kuondoka zake japo mazuri yake klabuni hapo yataendelea kukumbukwa tena na tena. Linaweza likawa ni pigo kubwa kwa Rais wa timu hiyo Florentino Perez lakini hakuna namna kwani kocha waliyempa kandarasi mpya klabuni hapo yupo nyuma ya kila kinachoendelea kwa sasa.
Ngoja tusubiri tuone………………
(0767 57 32 87)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni