Jumatano, 8 Julai 2015

COPA AMERIKA 2015: ILIKUWA NI FAINALI YA ALEXIS SANCHEZ NA LIONEL MESSI.


Na Oswald Ngonyani.

Dunia nzima ilikuwa kimya kushuhudia mchezo wa fainali wa Mashindano ya Copa America ambapo timu mwenyeji ya Chile ilikuwa inapambana na timu ya Taifa ya Argentina, mchezo ambao ulitabiriwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na uimara wa kila timu.
Haukuwa mchezo wa lelemama, ulikuwa ni mchezo ambao kila Taifa lilikuwa linataka kuweka heshima fulani, heshima ambayo mwisho wa siku ingeweza kuleta kumbukumbu ya pekee katika historia ya mchezo wa soka katika bara husika. Ilikuwa ni vita ya akina Lionel Messi, Angel Di Maria na wengineo dhidi ya akina Alexis Sanchez na wenzake waliokuwa wanaunda kikosi cha Chile.
Kunako mchezo huo uliopigwa Usiku wa kuamkia Jumapili iliyopota Chile walifanikiwa kuweka historia mpya kabisa wakiwa  nyumbani, baada ya kupata ushindi mnono wa goli 4-1, ushindi wa mikwaju ya penati na kutwaa ubingwa huo mkubwa katika ngazi ya mabara.
Hili ni kombe la kwanza kutwaa nyumbani katika historia ya soka yao, ambapo wakati Alexis Sanchez wa Arsenal aliyeng’ara tangu mwanzo akicheka hadi mwisho, Lionel Messi wa Argentina alikumbana na kigingi na hata kukumbwa na fadhaiko kuu ndani ya moyo wake.
Haikuwa mechi ya masihara, ilikuwa ni mechi iliyoonekana kuwa ngumu kwa kila timu na ndio maana dakika 90 za awali zilionekana kuwa ngumu kwa timu zote mbili, lakini hata zilipoongezwa dakika nyingine 30 bado milango ilionekana kuwa migumu na hivyo changamoto ya mikwaju ya penalti kuchukua nafasi yake.
Image result for lionel messi na alexis sanchez
(Alexis Sanchez akishangilia baada ya kuifungia timu yake bao la ushindi na kuipa ubingwa wa kwanza wa Kombe la Copa America)

Alikuwa ni Alex Sanchez aliyepeleka furaha nchini Chile  baada ya kupiga mkwaju wa ushindi na kushangilia kwa muda mrefu huku wenzake wakijumuika naye kumsapoti.
Usiku huo haukuwa mzuri kwa Higuain hii ni kutokana na ukweli kuwa katika dakika ya 90 alishindwa kufunga bao la wazi ambalo lingemaliza mchezo katika muda wa kawaida. Wakiwa suluhu walilazimika kucheza dakika 30 za nyongeza lakini hakuna aliyebahatika kufumania nyavu za mwenzake, lakini hata katika hatua ya matuta bado Higuin aliendeleza mkosi baada ya penalti yake kutoingia nyavuni.
Sanchez naye nusura afunge katika dakika za mwanzo za muda wa nyongeza lakini ilibidi wafike hatua za matuta ili mshindi aweze kupatikana. Ni Messi peke yake ndiye aliyeweza kutikisa nyavu za wapinzani, wanzake wote wala hawakuweza kufunga penati zao na hata kuzidi kumpa machungu mwanandinga huyo aliye na kiu ya kuipa mafanikio nchi yake.
Ikumbukwe kuwa Timu ya Taifa ya Argentina, au Le Albiceleste kama wanavyojulikana kwa utani, hawajatwaa taji kubwa kwa miaka 22 sasa, kwani mara ya mwisho walitwaa kombe hili walilobeba Chile nchini Ecuador mwaka 1993.
(Fainali ya Copa America mwaka huu 2015 ilifanyika hapa)
Kwa upande wa mabingwa wapya, hii ni mara yao ya kwanza kutwaa kombe hili katika kipindi cha miaka 99 na nusura imalizike karne pasipo kulitwaa. Hata hivyo, kutokana na uimara wa kikosi chao, wengi walisema wakikosa safari hii huenda ikabaki historia.
Chile ni moja ya timu zilizocheza mashindano haya kwa mara ya kwanza kabisa 1916 nchini Argentina lakini walichoweza kufanya vyema zaidi ilikuwa ni kupata ushindi wa pili, ambao wameutwaa mara nne; 1955, 1956, 1979 na 1987.
Kimahesabu ya mchezo wa soka ni kwamba akina Alexis Sanchez na Artulo Vidal wametwaa ubingwa huu baada ya kucheza mechi 173 katika mashindano yote, yaani tangu mashindano ya kwanza ya Copa America mwaka 1916.
Kunako mchezo huo Chile hawakucheza kwa kushambulia kama ilivyokuwa imezoeleka kabla, hii ilitokana na umaridadi wa kikosi cha Argentina, hivyo walichofanya ni kuwavuta Argentina, huku wakicheza kwa nidhamu ya hali ya juu lakini mara moja moja walifanya mashambulizi ya kushtukiza yalikuwa yanaongozwa na nyota wao  Sanchez na Charles Aranguiz.
Washabiki wao walikuwa wakishangilia mwanzo mwisho kwenye fainali hiyo kwa lengo la kuchagiza ushindi waliokuwa wameukosa kwa miaka mingi, walipeperusha bendera zao nyekundu ili kuwapa morali wachezaji wao waliokuwa wanacheza nyumbani.
 Kila timu ilifunga penati ya kwanza, Matias Fernandez akitia yake kwenye kona ya juu kwa Chile kabla ya Messi kuingiza yake kima cha chini kwenye kona.
Hata hivyo, baada ya kiungo wa Juventus, Arturo Vidal kupiga mkwaju mkali na kujaa wavuni kwa Chile, Higuain alipiga juu ya mwamba; Aranguiz akafanya mabao kuwa 3-1 ndipo Banega akazuiwa na Bravo huku Sanchez akicheka na nyavu na kuanza ‘shamra shamra’ ya aina yake ndani na nje ya uwanja.
(Kikombe cha ubingwa wa Copa America 2015 kilichokuwa kinagombaniwa katika fainali hiyo)
Ni kama kusema Argentina wamenyang’anywa tonge la pili mdomoni, baada ya mwaka jana 2014  kuukosa ubingwa wa dunia katika fainali ambazo kikosi chao kilionekana kuwa bora zaidi kama cha msimu huu, wajerumani walitamatisha ndoto zao baada ya Mario Goitze aliyeingia kipindi cha pili kucheka na nyavu kunako dakika za lala salama.
Bila shaka matokeo haya yameendelea kumuumiza sana Lionel Messi, mchezaji wa kiwango cha hali ya juu aliyechukua kila kikombe ndani ya Klabu yake ya Barcelona, kwa bahati mbaya hajafanya hivyo kwa timu yake ya Taifa. Bila shaka nyakati hizi huenda zikaathiri sana maisha yake ya ndani na nje ya uwanja.
NGOJA TUSUBIRI TUONE…….

(Maoni/Ushauri tuma kwenda 0767 57 32 87 au ngonyanioswald@gmail.com)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni