Alhamisi, 18 Juni 2015

MARADONA & PELE: WALIWAHI KUIKONGA DUNIA NA KUANDIKA ALAMA ISIYOFUTIKA KATIKA VICHWA VYA WAPENDA SOKA WENGI ULIMWENGUNI

Inaendelea kutoka Makala ya juzi……

DIEGO ARMANDO MARADONA
Image result for diego maradona

Diego Armando Maradona alizaliwa tarehe 30Mwezi  Oktoba 1960, ni mchezaji maarufu wa mpira wa miguu aliyewahi kuwika sana katika kikosi cha timu yake ya Taifa ya Argentina.
Ana urefu wa Mita 1.65 ambaye katika enzi zake za kusakata Gozi la ng’ombe alikuwa akicheza katika nafasi ya ushambuliaji wa kati. Katika nyakati fofauti yaani kati ya mwaka 1976 mpaka 1997 aliwahi kuvichezea vilabu vy Argentina Juniors, Boca Juniors, Barcelona, Napoli, Sevilla, na Newell’s Old Boys, huku akiwa tegemezi katika timu yake ya Taifa katika miaka ya 1977-1994.

Image result for diego maradona

Mchezo wa soka kama unavyojidhihirisha kwa kuwa na ubora wa hali ya juu na hata kujikusanyia mashabiki wengi kuliko michezo mingineyo umekuwa ni zaidi ya mchezo wa kawaida. Hauna tofauti  na sanaa. Kwa baadhi ya watu mchezo wa soka ni imani kama ilivyo imani nyingine za dini. Kuna watu akili na mawazo yao siku zote vimeathirika na soka.

Ndivyo ilivyo kwa wakazi wa Taifa la Argentina, Taifa ambalo kwayo mchezo wa soka hauna tofauti  na dini au imani.  Kwa wenyewe  mwanaume huyu ‘Diego Maradona’ ni kama Mungu wao. Mambo yote aliyowahi kuyafanya enzi zake za usakataji wa kabumbu na hata sasa baada ya kustaafu kwao ni mambo yaliyowekwa katika viriba vya ubongo wao na kamwe hawatakuja kuyasahau.

Ni kama kusema kuna wafuasi  wengi sana wa dhehebu la Maradona ndani na nje ya Argentina hususan Amerika. Diego Armando Maradona hana tofauti na nabii aliyetokea kupendwa sana lakini pia kuchukiwa sana na jamii ya wapenda soka ulimwenguni kote.  Hapa ndipo anapotofautiana na nguli mwingine wa kandanda, Pele wa Brazil.

Kwa jinsi ilivyo ni wazi kuwa hakuna shabiki wa soka atakayeweza kunipinga iwapo nitaandika sentensi hii ‘Ni wanasoka wachache sana katika ulimwengu huu wa kandanda waliotokea kuibua hisia za wapenzi wa mchezo huo kwa namna ya pekee kama ilivyo kwa Maradona’. Huo ndio ukweli.
Japo sikuzaliwa lakini takwimu za soka zinanifanya niweke bayana kuwa uwezo wa Maradona na umahiri wake katika kuuchezea mpira ulionekana wazi zaidi katika mwaka wa 1986 katika michuano ya Kombe la Dunia na hususan katika pambano la Argentina dhidi ya Uingereza.

Mpaka leo hii waingereza wamegoma kabisa kumsamehe  Maradona. Pengine wana sababu nyingi zinazowafanya wamjengee ‘bifu’ la milele  lakini sababu kubwa ni hii; Maradona alifunga goli la mkono, lakini baadaye kidogo Maradona alifunga goli la kiufundi na la utalaamu wa hali ya juu zaidi pale alipoambaa kwa kasi na mpira akitokea nusu ya uwanja.

Image result for diego maradona
Jemedari huyu aliwapiga chenga za maudhi karibu wachezaji wote wa Uingereza waliomkabili. Kisha aliukwamisha mpira kimiani. Kilikuwa ni kitendo cha aibu kubwa sana kwa wachezaji wa Uingereza kwao ni kama aliwafedhehesha na hata kuonekana si kitu mbele ya halaiki ya mashabiki wao waliojitokeza kuangalia mchezo huo nchini Mexico.

Maradona alidhihirisha umahiri wake katika sanaa ya kandanda, sanaa inayoongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wafuasi. Itakumbukwa, kuwa Argentina ilishinda Kombe la Dunia mwaka ule., ni wazi kuwa goli la mkono lilichagiza kuivusha Argentina katika hatua iliyofuata, mpaka leo waingereza bado wana kinyongo na nabii huyu wa soka.

Miaka minne baadae, juhudi binafsi za Maradona ziliiwezesha nchi yake kushika nafasi ya juu zaidi katika michuano ya Kombe la Dunia. Huu ni ukulu mwingine wa Maradona, ukulu ambao unamfanya azidi kuheshimika zaidi katika mawanda ya kandanda.

Katika fainali zile mechi kati ya Brazil na Argentina ndiyo iliyokuwa na kivutio cha pekee. Brazil waliwazidi Argentina katika idara zote, hivyo basi, Argentina na Maradona wao wala haikupumua. Lakini ajabu iliyoje, kama radi, kama gharika, Mwanamume huyu alizinduka na kuishangaza dunia ya wapenda soka wengi duniani waliokuwa wakifuatilia mchezo ule.

Akiwa amebanwa katika kila upande huku akikabwa na walinzi wa Brazil, Maradona alifanikiwa kutoa pasi muhimu katika maisha yake ya yote ya kisoka.Ilikuwa pasi murua kwa mchezaji mwenzake, Claudio Caniggia ambaye alifunga goli pekee katika mchezo huo.

Argentina waliingia fainali na kushindwa mbele ya wababe wengine wa soka ‘Ujerumani’. Kama hiyo haitoshi, Fainali za Kombe la Dunia za mwaka 1994 zilimshuhudia Maradona akiwa katika hatua za kuporomoka kisoka. Nabii huyu wa soka sasa likuwa ameanza kupoteza mvuto.
Alijitahidi kidogo katika mechi za awali, kisha likalipuka bomu lililomharibia kabisa sifa yake ya kuwa juu kisoka na hata kumpa mwanya mpinzani wake, Edson Pele kuonekana bora zaidi kuliko yeye.
Maradona alibainika kutumia vidonge vya kuongeza nguvu aina ya efedrin. Argentina nayo ikapoteza mvuto mbele ya washika dau wengi wa kandanda lakini pia haikufanya cha maana katika hatua za awali za fainali hizo.
Image result for diego maradona

Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Nabii Maradona, nabii wa soka anayezungumzwa zaidi mpaka sasa. Soka kama dini ina wafuasi wengi sana ambao si rahisi kuwahesabu. Siku zote bila mpira uwanjani hakuna soka. Kama ulivyo mpira wenyewe, una umbo la mviringo, wenye sura nyingi zisizoelezeka na wenye kudunda, basi hata pambano lenyewe la soka laweza kuwa na sura nyingi. Ndiyo maana watu husema Mpira unadunda, hii maana yake ni kwamba katika soka lolote laweza kutokea.

Soka, kandanda, kabumbu, kipute au ndinga. Yote hayo na mengineyo ni majina yenye kuzungumzia aina moja ya mchezo ambao si mchezo mwingine bali ni mpira wa miguu.  Kwangu mchezo huu ni kama mchezo wa maajabu, Tazama, katika mchezo huu mchezaji anaruhusiwa kutumia sehemu nyingine zote za mwili, kichwa, kifua, tumbo,  makalio,mgongo, kisigino na hata kidevu, lakini kamwe haruhusiwi kutumia mkono.

Tofauti na michezo mingine kama Wavu, Kikapu, Mpira wa meza na mingineyo mingi ambapo mikono hupewa kipaumbele zaidi katika kila mchezo. Ajabu iliyoje, Ni dhambi kubwa sana katika soka kwa mchezaji wa soka kuucheza mchezo huo kwa kutumia mkono na kibaya zaidi akifanya hivyo kwa kudhamiria, kwa makusudi. Dhambi hiyo haisameheki katika soka, adhabu yake ni kutolewa nje kwa kadi nyekundu. Mkono ni Ibilisi wa soka.

Ndio maana mpaka leo hii, Waingereza hawatakoma kumlaani Diego Maradona wa Argentina kwa kufunga goli lile la mkono nililolielezea  katika aya za mwanzoni.

Kwa Waingereza, Maradona alifunga goli kwa kumtumia Ibilisi wa soka, wana haki ya kumlaumu kwani safari yao nchini Mexico katika mwaka ule (1986) iliishia hapo kwa goli la mkono wa Maradona.

Image result for diego maradona

Maradona mwenyewe alitoa kauli ambayo ilizidi kuwanyong’onyesha Waingereza alipodai kuwa lilikuwa goli la mkono wa Mungu!


(0767 57 32 87)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni